Saturday, 16 April 2016

Lugumi pasua kichwa



Waziri wa Mambo ya ndani Charles Kitwanga.

SAKATA la ufisadi kuhusu mkataba kati ya Kampuni ya Lugumi Enterprises Ltd na Jeshi la Polisi nchini sasa limechukua sura mpya huku moja ya kampuni kubwa ya Marekani ikitajwa.

Hatua hiyo imekuja huku kukiwa na utata kuhusu mkataba huo ambapo sasa Kampuni ya Biometrica LLC ya Marekani ikihusishwa na sakata hilo.

Inaelezwa mwaka 2011, Kampuni hiyo ya Kimarekani iliwasilishwa na Kampuni ya Teknolojia ya Infosys IPS Tanzania Limited, ambapo waliingia nayo mkataba wa kufunga baadhi ya mashine hizo za kuchukua alama za vidole katika vituo vya polisi nchini.

Baada ya kukamilika kwa kazi hiyo bado haijatajwa ni vituo vingapi Infosys Tanzania Limited ilifunga mashine hiyo.

Akizungumzia mkataba huo, Naibu Meneja Mkuu wa Infosys, Sweki Donald, alisema wakati wote wakiwa wanaendelea na kazi hawajawahi kushirikiana na Kampuni ya Lugumi Enterprises.

“Mwaka 2011 tulipata kazi ya kufunga mashine za kuchukua alama za vidole katika vituo vya polisi na kazi hii sisi tuliipata kupitia Kampuni ya Biometrica LLC ya nchini Marekani ambao wao walisema wamepata taarifa zetu kupitia Kampuni ya Dell ya Marekani.

“Tulifanyakazi yetu kwa mujibu wa mkataba na baada ya kumaliza tulilipwa Dola 74, 420 (sawa na shilingi 162,849,565), ila ninapenda kusema kuwa wakati wote hatukujua kama kuna mtu anaitwa Lugumi.

“Tumekuja kujua baadaye sana hivyo ninapenda kusema hapa kuwa hatuhusiki na Lugumi na wala hatumjui,” alisema Sweki wakati wa mahojiano na mwandishi aliyejitambulisha wa Focus Media.

Naibu Meneja huyo alipoulizwa kuhusu ushiriki wa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga, alisema waziri huyo alikuwa ni mmoja wa waasisi wa kampuni hiyo ingawa aliondoka tangu mwaka 2010.

“Charles Kitwanga ni mmoja wa founder wa Infosys Tanzania Limited, tangu mwaka 2010 aliondoka katika kampuni na amekuwa hana mawasiliano,” alisema Sweki.

Alisema wao kama Infosys Tanzania Limited, hawahusiki na kashfa ya ufisadi huo unaoripotiwa sasa.
Katika kile kinachoonekana ni filamu hasa baada ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), kutoa siku tatu kwa kampuni hiyo kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa mradi wa kufunga mashine za utambuzi wa alama za vidole katika vituo 108 nchini, sakata hilo limekuwa likichukua sura mpya kila kukicha.

Uamuzi huo uliibua hisia miongoni mwa jamii ambapo katika kipindi cha siku mbili baada ya PAC kutaka ripoti hiyo, Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, iliingilia kati ambapo mwenyekiti wake Balozi Adadi Rajabu, alikiri kupokea mkataba huo.

Hali hiyo ilizua sintofahamu miongoni mwa wajumbe wa Kamati za Bunge huku baadhi yao wakihofu hatua hiyo huenda ikawa ni mkakati wa kuficha ukweli dhidi ya vigogo waliotajwa katika mkataba huo tata wa Sh bilioni 37.

Kauli ya Bunge
Pamoja na jana kuwa ni siku ambayo ilitarajiwa kampuni hiyo ingewasilisha, hatimaye jana Ofisi ya Bunge kupitia Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano, ilieleza kuwa taarifa hiyo itawasilishwa Aprili 18, mwaka huu.

Taarifa hiyo ilieleza kwamba tangu lilipoibuliwa sakata hilo na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Aprili 5, mwaka huu baada ya Jeshi la Polisi kutakiwa kuwasilisha mkataba  ulioingiwa kati ya Jeshi hilo na Kampuni ya Lugumi Enterprises Ltd kuhusu mradi wa Utambuzi wa Alama za Vidole AFIS (Automated Fingerprint Identification System), kumekuwa na taarifa ambazo si sahihi.

“Ukweli kuhusu jambo hili ni kwamba, Aprili 5 mwaka huu, kamati hiyo ilikutana na kujadili taarifa ya Ukaguzi wa Hesabu zilizokaguliwa za fungu 28, Jeshi la Polisi kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, 2014 ambapo kamati pamoja na mambo mengine ilibaini dosari katika utekelezaji wa mkataba huo.

“Kutokana na dosari hizo, kamati iliomba Ofisa Masuhuli ambaye ni Katibu Mkuu wa  Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuwasilisha maelezo ya kina kwa maandishi kuhusu utekelezaji wa mradi huo kwa Ofisi ya Katibu wa Bunge ili kamati iweze kuchambua na  kujadili maelezo hayo kabla ya kupendekeza kwa Bunge hatua zaidi za kuchukua.

“Kutokana na agizo hilo, kamati ilimwandikia pia Katibu wa Bunge taarifa kuhusu agizo hilo Aprili 12 mwaka huu, ili kupatiwa maelezo hayo kutoka kwa Ofisa Masuhuli. Aidha, Ofisi ya Bunge ilimwandikia barua Katibu Mkuu, Wizara ya Mambo ya Ndani Aprili 12 mwaka huu kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa maagizo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) iliyotokana na kikao hicho cha Aprili 5 mwaka huu kabla ya Aprili 18 mwaka huu kama ilivyoshauriwa na kamati,” ilieleza taarifa hiyo.

Sarakasi zaidi
Kampuni ya Lugumi Enterprises Ltd inadaiwa kupewa tenda na Jeshi la Polisi kwa ajili ya kufunga mashine za kuchukua alama za vidole katika vituo 108 nchi nzima kwa gharama ya Sh bilioni 37.

Hadi sasa mashine hizo zimefungwa katika vituo 14 vya polisi pekee na tayari kampuni hiyo imelipwa Sh bilioni 34 ambazo ni sawa na asilimia 99 ya fedha za mkataba.

Kamati ya PAC ambayo ilibaini kuwapo viashiria vya ufisadi katika zabuni, iliwaagiza watendaji wa jeshi hilo kuwasilisha taarifa za mkataba huo, lakini mkataba huo ulihamishwa na kupelekwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Lugumi ambaye anatajwa kuwa na uhusiano wa kifamilia na baadhi ya vigogo nchini, aliingia mkataba tata na Jeshi la Polisi mwaka 2011 kwa ajili ya kufunga mashine za kuchukua alama za vidole katika vituo vya polisi, lakini kazi hiyo haikufanyika kwa ufanisi licha ya kulipwa mabilioni ya fedha.

Chanzo cha kuaminika kililiambia gazeti hili kuwa mfanyabiashara huyo amekwenda nje kununua mashine zilizosalia kama njia ya kuzima mjadala kuhusu utata wa mkataba huo ambao unaelezwa kumhusisha kigogo mmoja katika Serikali ya Rais Dk. John Magufuli.

Utata
Katika sakata hilo inadaiwa kuwa Kampuni ya Lugumi Enterprises ilipewa zabuni ya kufunga mashine za ‘Biometric Access’ kwa ajili ya kuchukua alama za vidole ikiwa haina uzoefu wa kazi hiyo.

“Wamepewa mkataba sawa, lakini mbona taarifa zinaonyesha kuwa kampuni hii haijasajiliwa kama Biometric Access Company na haijawahi kufanya kazi zozote zinazohusiana na Biometric Access Control?” alihoji mmoja wa wataalamu ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.
CHANZO: MTANZANIA.

Friday, 15 April 2016

Nchi za kiislamu zanuia kupunguza migawanyiko ya kimadhehebu


Viongozi wa nchi wanachama wa Jumuiya ya OIC.

Rais wa Uturuki Tayyip Recep Erdogan anahitimisha mkutano wa viongozi wa nchi za kiislamu unaolenga kupunguza tofauti za kimadhehebu hasa kuhusu mizozo ya Syria na Yemen na kushughulikia kitisho cha ugaidi. 

Katika dhifa ya chakula cha jioni hapo jana aliyowaandalia viongozi wa nchi za kiislamu wanaohudhuria mkutano huo wa kilele wa jumuiya ya ushirikiano ya mataifa ya Kiislamu OIC, Rais Erdogan amekariri haja ya kuwepo umoja na mshikamano miongoni mwa waislamu wote.

Erdogan amesema lengo ni kuwapa waislamu matumaini kuhusu siku za usoni na kutokana na mkutano huo, wanatarajia ukurasa mpya utafunguliwa.

Miongoni mwa viongozi waliohudhuria mkutano huo wa OIC ni Mfalme Salman wa Saudi Arabia na Rais wa Iran Hassan Rouhani ambao nchi zao zimekuwa zikitofautiana vikali na kuchukua misimamo tofauti kuihusu mizozo ya Yemen na Syria.

Wasunni na Washia wahimizwa kupendana
Rais Rouhani ambaye pia alizungumza katika mkutano huo amesema hakuna ujumbe ambao unachochea mgawanyiko miongoni mwa Waislamu unapaswa kutolewa katika mkutano huo.

Uturuki inayoutazama mkutano huo kama jukwaa la kuinua hadhi yake katika ulimwengu wa kiislamu pia nchi hiyo imepata fursa ya kuwaleta pamoja waislamu takriban bilioni 1.7 kutoka duniani.

Erdogan ambaye nchi yake inashikilia wadhifa wa uenyekiti wa OIC kwa kipindi cha miaka miwili ijayo anatarajiwa kuongoza kikao cha mwisho cha mkutano huo ulioanza tangu jana leo kabla ya kufanya mkutano na wanahabari.

Viongozi hao wa nchi takriban 30 za kiislamu wamekubaliana kushirikiana zaidi katika kupambana dhidi ya ugaidi na uhalifu mwingine na kuundwa kwa kituo cha kushughulikia ushirikiano zaidi wa polisi wa nchi wanachama wa OIC ambacho kitaanzishwa Istanbul.

OIC ina nchi wanachama 57
Mkutano huo wa OIC unakuja wakati ambapo Uturuki inaonekana kutafuta ushirikiano zaidi na Saudi Arabia. Hapo jana mawaziri wa mambo ya nje wa nchi hizo mbili walitia saini makubaliano ya maelewano kuhusu kuundwa kwa baraza la ushirikiano wa nchi hizo mbili.

Uturuki, Saudi Arabia na Qatar zinawaunga mkono waasi wanaompinga Rais wa Syria Bashar al Assad. Kwa upande mwingine Iran na Urusi ambayo ina uhusiano mbaya katika siku za hivi karibuni na Uturuki zinauunga mkono utawala wa Rais Assad.

Wachambuzi wameonya kuwa Uturuki inapaswa kutahadhari kuhusu ushirikiano wake na Saudi Arabia ili isije ikaonekana kuwa na uhusiano wa misingi ya kimadhehebu unaoilenga Iran.

Katika hatua ya Uturuki kujaribu kusawazisha hali, Rais Rouhani anatarajiwa kuanza ziara rasmi Uturuki ya kuimarisha uhusiano kati ya Iran na Uturuki punde baada ya kukamilika kwa mkutano huo wa kilele wa OIC. Shirika hilo la ushirikiano wa mataifa ya kiislamu lina wanachama 57.
CHANZO: DW.

Mapya ya Lugumi


IGP Ernest Mangu.

WAKATI leo Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), ikitarajiwa kupokea mkataba tata wa Jeshi la Polisi na Kampuni ya Lugumi Enterprises Ltd, mapya yameibuka katika sakata hilo.

Kampuni hiyo inadaiwa kupewa tenda na Jeshi la Polisi kwa ajili ya kufunga mashine za kuchukua alama za vidole katika vituo 108 nchi nzima kwa gharama ya Sh bilioni 37.

Hadi sasa mashine hizo zimefungwa katika vituo 14 vya polisi pekee na tayari kampuni hiyo imelipwa Sh bilioni 34 ambazo ni sawa na asilimia 99 ya fedha za mkataba.

Kamati ya PAC ambayo ilibaini kuwapo viashiria vya ufisadi katika zabuni, iliwaagiza watendaji wa jeshi hilo kuwasilisha taarifa za mkataba huo, lakini mkataba huo ulihamishwa na kupelekwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Hata hivyo mfanyabiashara anayemiliki kampuni ya Lugumi Enterprises, Said Lugumi anadaiwa kukimbia nchi, huku mkataba wake na Jeshi la Polisi ukipigwa danadana katika Kamati za Bunge.

Taarifa za kukimbia kwa mfanyabiashara huyo anayetajwa kuwa na ukwasi wa kupindukia katika kipindi kifupi, zilielezwa na baadhi ya maofisa wa vyombo vya dola, ambapo anadaiwa kuwa alitoweka nchini usiku wa Jumatatu ya wiki hii.

Wakati Lugumi akidaiwa kukimbia nchi, taarifa nyingine zilizolifikia gazeti hili jana zinaeleza kuwa, mfanyabiashara huyo amekwenda nje ya nchi kununua mashine 94, ambazo bado hazijafungwa katika vituo vilivyosalia, ili kukamilisha idadi ya vituo 108.

Lugumi anayetajwa kuwa na uhusiano wa kifamilia na baadhi ya vigogo nchini, aliingia mkataba tata na Jeshi la Polisi mwaka 2011, kwa ajili ya kufunga mashine za kuchukua alama za vidole katika vituo vya polisi, lakini kazi hiyo haikufanyika kwa ufanisi licha ya kulipwa mabilioni ya fedha.

Chanzo cha kuaminika kililiambia MTANZANIA kuwa mfanyabishara huyo amekwenda nje kununua mshine zilizosalia, kama njia ya kuzima mjadala kuhusu utata wa mkataba huo, ambao unaelezwa kumhusisha kigogo mmoja katika Serikali ya Rais Dk. John Magufuli.

“Lugumi amekwenda nje lakini hakutaka watu wajue na kaenda kununua vifaa ili wamalize kazi kwa Supersonic Speed and put (kwa kasi) kama njia ya kufunga mjadala,” kilisema chanzo chetu.

Juzi chanzo kimoja kililiambia MTANZANIA kuwa, mfanyabiashara huyo amekuwa akitembea na msafara mkubwa wa magari ya kifahari, huku akilindwa na walinzi maalumu wa kukodi alitoroka nchi wakati vyombo vya dola vikimuwinda.

“Ninashangaa vyombo vya habari mnashupalia Lugumi, Lugumi… mbona sasa ana siku ya tatu ameondoka nchini. Na inaweza kuwa amekwenda mafichoni.

“Pamoja na hali hiyo, lakini bado tunaendelea kumsaka ingawa baadhi ya idara zinazohusika na vyombo vya dola zimefanikiwa kufanya mahojiano naye ya kina kuhusu suala la mkataba wake wa kufunga mashine za kuchukua alama za vidole katika vituo vya polisi,” alisema mtoa habari huyo.

Licha ya Kampuni ya Lugumi kuingia mkataba na Jeshi la Polisi wa Sh bilioni 37, lakini bado mfanyabiashara huyo alilipwa Sh bilioni 46 nje ya mkataba, jambo linalozidi kufikirisha na kutilia shaka juu ya zabuni hiyo.

Sakata hili lilibainika wiki iliyopita baada ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), kukutana na maofisa wa jeshi hilo kupitia taarifa ya hesabu zao za mwaka 2013/14 zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Utata
Katika sakata hilo inadaiwa kuwa Kampuni ya Lugumi Enterprises ilipewa zabuni ya kufunga mashine za ‘Biometric Access’ kwa ajili ya kuchukua alama za vidole ikiwa haina uzoefu wa kazi hiyo.

“Wamepewa mkataba sawa, lakini mbona taarifa zinaonyesha kuwa kampuni hii haijasajiliwa kama Biometric Access Company na haijawahi kufanya kazi zozote zinazohusiana na Biometric Access Control?,” alihoji mmoja wa wataalamu ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.

Pamoja na PAC kutaka mkataba huo, lakini katika hali ya kustaajabisha hoja hiyo iliandaliwa mazingira ya kuhamishwa na kupelekwa katika Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, ambapo mwenyekiti wake, Balozi Adadi Rajabu, alikiri mkataba huo kuwasilishwa mbele ya kamati yake.

“Mimi kama mwenyekiti wa kamati ninapenda kukiri kwamba tumepokea mkataba kati ya Jeshi la Polisi na Kampuni ya Lugumi na tutaufanyia kazi kwa kina.

“Tunahitaji kuona kama kuna wizara zilizohusika na mkataba huu na kama tutaukuta ni mbaya, tutatoa taarifa kwa umma. Kikubwa tunawaomba Watanzania wawe watulivu, hatuko kwa ajili ya kumlinda mtu wala kikundi cha watu, tunasimamia masilahi ya Watanzania wote,” alisema Balozi Adadi alipozungumza na gazeti hili juzi.

Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa, wamekuwa wakihoji sababu za mkataba huo kuhamishwa, wakati Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama haihusiki na masuala ya fedha.

“Ukitazama sakata hili, the main issue (jambo la msingi) ni fedha zilizochukuliwa ukilinganisha na kazi iliyofanywa, suala hapa si mashine za vidole hoja ni fedha.

“Kwa msingi huo, Kamati ya PAC ndiyo yenye jukumu la kukagua hesabu za Serikali, tangu lini Kamati ya Mambo ya Nje ikashughulika na hesabu?

“Wao kazi yao ni kuangalia diplomasia na masuala ya usalama, sisi hatuko huko shida yetu tunataka kujua kuhusu fedha za umma zilizopigwa mchana kweupe,” alisema mchambuzi mmoja ambaye hakutaka jina lake litajwe.
CHANZO: MTANZANIA.

Rais tumbua majipu lakini usisahau…..(1)



Joseph Mihangwa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt, John Pombe Magufuli.

Na Joseph Mihangwa.
SI siri tena kwamba Tanzania imegubikwa na ufisadi wa kutisha, mkubwa na wa aina yake Afrika Mashariki kama si barani Afrika.

Ufisadi huu, ulioanzia Serikali ya Awamu ya Pili, chini ya Rais Ali Hassan Mwinyi kwa kubinafsisha kila kitu kilichokuwa cha umma, kwa usiri mkubwa, mizengwe na kwa bei ya kutupa, uliongeza kasi wakati wa Serikali ya Awamu ya Tatu, chini ya Rais Benjamin William Mkapa.

Walifanya hivi kwa njia ya uwekezaji tata na usiojali, ambapo wawekezaji walipewa (kukalia) kiti cha mbele katika uchumi wa taifa, kwa mikataba ya uwekezaji mibovu iliyowaruhusu kupora watakavyo, kiasi cha nchi yetu kugeuzwa “Shamba la Bibi”

Kipindi hicho, tumeshuhudia kashfa kubwa kubwa za ufisadi zenye kuatamiwa kwa machukizo ya Umma, kama ile ya Independent Power Tanzania Ltd (IPTL/TANESCO), ambapo nchi imeporwa mabilioni ya fedha kwa mkataba wa umeme tata wa miaka 20 kuanzia mwaka 1999.

Chini ya mkataba huu, nchi imetupwa gizani kwa kukosa umeme, lakini inaendelea kuilipa IPTL zaidi ya Shs. 5bn/= kwa mwezi bila kujali, umeme uwepo au usiwepo; tutumie au tusitumie, kwa sababu mkataba huo mbovu uliofikiwa mwaka 1995 unaelekeza hivyo.

Walioliingiza Taifa katika “mkenge” huu wanafahamika kwa vyeo na kwa majina; lakini wapo huru wanapeta.

Kashfa zingine zenye kuangamiza ustawi wa taifa ni pamoja na zile za EPA, ununuzi wa rada na ndege ya Rais; ubinafsishaji wa NBC na uuzaji wa nyumba za serikali; Mgodi wa makaa ya mawe wa Kiwira, Richmond/Dowans, mikataba mibovu ya madini; Loliondo, na ufujaji wa zaidi ya bilioni 800/= za mfuko wa kuwezesha uagizaji bidhaa (CIS), kwa kutaja kashfa chache tu.

Na kama tusingeshtuka, manyang’au hawa walikuwa wamepania pia kuhujumu mifuko ya akiba ya wafanyakazi kwa kujichotoa mabilioni ya fedha kwa njia ya ushiriki katika vitega uchumi vya mifuko hiyo

Na ingawa ufisadi huu unafahamika vizuri, na wahusika wanajulikana kwa serikali (ikiwamo serikali ya awamu ya nne), juhudi zimeendelea kufanywa kuatamia uchafu huo, na wahusika kuoshwa kwa sabuni kali ili, kwa hadaa kubwa, waweze kumeremeta machoni mwa umma.

Kwa mifuko ya Hifadhi ya Jamii, tunayo mifano kadhaa: mwaka 1996 Waziri Mkuu wa wakati huo, kwa kutumia nafasi yake, aliweza kukopeshwa shs. 57m/= kutoka Mfuko wa Pensheni wa Watumishi wa Umma (PPF) nje ya sera na taratibu za ukopeshaji za mifuko ya hifadhi ya Jamii nchini na duniani kote.

Vivyo hivyo, mwaka 2006, mfanyabiashara mmoja maarufu Jijini Dar Es Salaam (jina tunalo), alikopa kutoka Shirika la Hifadhi ya Jamii Nchini (NSSF) kwa taratibu za kutatanisha, Shs. 9bn/= kwa ajili ya kukarabati maghala yake, na baadaye kuiuzia NSSF maghala hayo kwa bei ya shs. 47bn/=, bei ambayo hata wathamini majengo wa serikali iliwaacha mdomo wazi.

Hakuishia hapo; mwaka huohuo, na katika kipindi hicho hicho; mfanyabiashara huyo, aliuuzia Mfuko wa Pensheni wa Watumishi Serikalini, maghala mengine kwa bei ya Shs. 39bn/= ambayo, kwa mujibu wa wathamini wa serikali, ilikuwa juu maradufu ya bei halisi ya mghala hayo.

Hizo ndizo zilikuwa enzi za mwanzo kabisa za utamaduni wa kukwapua mali ya umma mingoni mwa wanasiasa na watawala, kwa kushirikiana na kada ya wafanyabiashara, kuota mizizi.

Utafiti makini umeonesha kwamba, katika juhudi za kujiponya, wahujumu hao ama walikimbilia kunyakua (kupora) nafasi za kisiasa wapate kinga ya kisiasa, au waligeuka kuwa wafadhili wakubwa wa chama tawala na kampeni za uchaguzi ili walindwe na kusafishwa. Janja yao hii imeweza kufanikiwa japokuwa kwa muda; wakajiona wako salama wakati usalama wa kweli haupo.

Lakini pamoja na hayo, licha ya chama na serikali kujitahidi kuzisafisha kashfa mbalimbali za ufisadi ziweze kumeremeta, kashfa moja kabambe nchini, ya mradi wa Mgodi wa Meremeta imeshindwa kumeremeta, na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuitaka Serikali iwasilishe hesabu za kampuni hiyo kwa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), zikaguliwe ili kukata mzizi wa fitina.

Kampuni ya Meremeta, ambayo inadaiwa kutosajiliwa chini ya Ofisi ya Hazina kama kampuni au shirika, ilichota malipo tata zaidi ya Shs. 155bn/= zilizolipwa na Benki Kuu (BOT) kwa kampuni ya Nedcor Trade Service, baada ya udhamini wa kampuni yenye hisa ya Triennex (PTY) Limited ya Afrika Kusini. Malipo haya na mengine, kama tutakavyoona badaye, ndiyo yaliyozua utata na Bunge kuagiza mahesabu yakaguliwa.

Katika makala haya, tutaona na kufahamu kama ni kweli kampuni ya Meremeta ni ubia wa serikali na kampuni ya Triennex, unaohusisha Jeshi letu la Ulinzi, kama inavyodaiwa, na pia kuhusisha usalama wa taifa. Tutaona ni kwa vipi, makampuni mengine kama Deep Green Finance na Tangold (yanavyoguswa na kashfa hii) yalivyoingia; na kwa nini serikali inajiuma mdomo na kukunja mikono yanapotajwa.

Lakini ifahamike kwa misingi ya sheria kwamba, kitendo cha mtu kufunika kombe au kuatamia kosa lililotendwa na mtu mwingine, kwa lengo la kumwepusha mtu huyo mwingine sheria isichukue mkondo wake dhidi ya mtu huyo; au kosa alilotenda lisijulikane, kinamfanya mtu huyo mwenye kutaka kumwokoa huyo mtu mwingine na yeye kuwa mshiriki wa kosa hilo kwa kiwango sawa na cha mtuhumiwa halisi wa kosa.

Kwa hiyo, viongozi wanaowalinda au kuwasafisha mafisadi wana hatia ya ufisadi uleule wa wale wanaojaribu kuwaokoa.

Huu ndio utamaduni wa kulindana kwa maovu, unaoshika kasi nchini kwa machukizo ya umma; kana kwamba viongozi na washirika wao wana kinga ya kimsahafu (Luka 12:32) kwamba, “Msiogope, enyi kundi dogo; kwa kuwa baba yenu (mfumo wa kifisadi) ameona vema kuwapa ule ufalme - (wa ulaji?)”

Kampuni ya Meremeta iliandikishwa na kusajiliwa nchini Uingereza Agosti 9, 1999 (kwenye kisiwa cha Isle of Man) na kupewa namba ya Usajili 3424504; lakini serikali yetu inadai ni ubia kati ya serikali ya Tanzania yenye asilimia 50 ya hisa, na Kampuni ya Triennex ya Afrika Kusini, inayomiliki hisa asilimia 50 pia.

Utata unaongezeka pale inapodaiwa kuwa, Makampuni ya London Law Serivices Ltd, na London Law Secretarial Ltd, nayo ni wanahisa wa Meremeta.

Madhumuni ya kampuni hiyo yalielezewa kuwa ni kununua dhahabu kutoka kwa wachimbaji wadogowadogo nchini, pamoja na kuwasaidia zana za kufanyia kazi. Swali linalojitokeza hapa ni kwa vipi kampuni inayomilikiwa na serikali, na ambayo shughuli zake zinafanyika hapa hapa nchini na kwa misingi ya usalama wa taifa, iandikishwe na kusajiliwa katika nchi ya kigeni?.

Kati ya mwaka 2003 na 2005, kampuni hii ilitelekeza wajibu na “madhumuni” ya kuanzishwa kwake na kuanza kuchimba dhahabu yenyewe huko Buhemba, Musoma. Hapo ndipo hadithi ya Meremeta kuhusisha usalama wa taifa ilipoanza; hapo ndipo hadithi ya Meremeta kujihusisha kusaidia kiwanda cha magari cha Jeshi cha Nyumbu (Pwani) ilipoanza kupikwa na kusikika.

Ikumbukwe kuwa, katika kipindi hicho (2003 – 2005), kiwanda cha Nyumbu kilipangiwa fedha kutoka serikalini jumla ya Sh. Milioni 950 kwa ajili ya kutengeneza magari 21 ya kijeshi, kwa wastani wa 45.2m/= kwa kila gari, na hakukuwa na fedha zaidi zilizoingia kutoka vyanzo vingine kipindi hicho.

Ukweli juu ya kwamba mradi wa Meremeta haukuhusika kwa namna yoyote ile na Jeshi la Wananchi, unathibitishwa pia na Waziri wa Ulinzi, Philemon Sarungi, katika hotuba yake ya bajeti ya 2004/2005, aliposema: “Mradi wa Buhemba umejengwa katika eneo lililokuwa Kambi ya Jeshi, na shughuli za uchimbaji na uzalishaji zinasimamiwa na Idara ya Madini”.

Kile tu kwamba mradi huo ulijengwa mahali ambapo zamani ilikuwa Kambi ya Jeshi, hakiufanyi uwe mradi wa Jeshi wenye kuhusishwa na Usalama wa Taifa. Ukweli ni kwamba, mgodi mpya wa Buhemba ulijengwa kwa Rand milioni 240 (dola 56m) na Kampuni ya WBHO (Pty) Ltd ya Afrika Kusini, na ulikamilika mwaka 2000. Ujenzi huo ulifanywa kwa niaba ya Meremeta na Triennex (kampuni zote tata), na si kwa niaba ya Serikali ya Tanzania. Ulizihusisha pia kampuni za Kigeni za Jefferies and Green na Time Mining, zote za Afrika Kusini.

Niharakishe kusema hapa kwamba, mmoja wa wanahisa wakubwa wa kampuni ya Time Mining ™, alikuwa Anna Muganda, mke wa aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Daudi Balali, ambaye ndiye pia aliyeileta kampuni hiyo nchini kuja kusimamia na kuendesha mgodi wa Meremeta, eti kwa niaba ya Serikali ya Tanzania.

Cha kushangaza hapa pia ni kwamba, wengi wa watumishi wa nje (expatriates) wa kampuni ya Ukaguzi ya Alex Stewarts ya mjini Washington, iliyoletwa Tanzania na Daudi Balali kukagua mauzo ya nchi za nje ya dhahabu kwa makampuni ya madini nchini, ndio haohao waliokuwa watumishi pia wa kampuni ya Time Mining ya Anna Muganda.

Kama kweli serikali ilikuwa na maslahi katika Meremeta, kwa nini iliruhusu mtu binafsi (Anna Muganda) kusajili kampuni binafsi ya kigeni kusimamia mradi huu? Na Daudi Balali alikuwa na mamlaka gani kuajiri kampuni binafsi kukagua uzalishaji na uuzaji nchi za nje, madini ya nchi hii, na kwa manufaa ya nani?.
…..Itaendelea toleo lijalo…..