Monday, 23 June 2014

Wabunge saba watikisa Bunge

Mbunge wa Singida Mashariki Mh. Tundu Lissu (CHDEMA).
Dodoma. Wabunge saba wamelitikisa Bunge tangu mkutano wa Bunge la Bajeti ulipoanza kutokana na michango yao binafsi.

Mwandishi wetu ambaye amekuwa bungeni tangu Mkutano wa Bajeti ulipoanza ametoa tathmini yake kuhusu michango ya wabunge iliyosisimua katika mjadala na kuibuka na orodha ya wabunge hao saba.


Hata hivyo, katika tathmini hiyo, majina ya wabunge ambao walichangia kwa niaba ya kamati au kutokana na nafasi zao za uwaziri au uwaziri kivuli hajayaingizwa katika orodha hiyo.

Tathmini hiyo imefanyika huku leo mjadala wa Bajeti ya Serikali ya 2014/15 ukihitimishwa tayari kwa kupigiwa kura na wabunge kesho, baada ya kukamilisha mfululizo wa mijadala ya bajeti za wizara zote za Serikali tangu Bunge hilo lilipoanza Mei 6, mwaka huu.


Hoja zilizoibuliwa na wabunge hao kwa nyakati tofauti ziliitikisa Serikali na kusababisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kiti cha Spika au aliyekuwa akikaimu nafasi ya Waziri Mkuu bungeni, Profesa Mark Mwandosya ambaye ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu) kusimama kutoa ufafanuzi.

Waliotikisa
Wabunge waliotikisa Serikali katika michango yao ni Ally Keissy (Nkasi Kaskazini - CCM), David Kafulila (Kigoma Kusini - NCCR-Mageuzi), Kangi Lugola (Mwibara - CCM), Dk Faustine Ndugulile (Kigamboni - CCM), Tundu Lissu (Singida Mashariki - Chadema), Abbas Mtemvu (Temeke –CCM) na Cecilia Paresso (Mbunge wa Viti Maalumu-Chadema) .

Kafulila
Siku mbili baada ya Bunge kuanza Mei 8 mwaka huu, wakati wa Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Kafulila aliibuka na sakata la kuchotwa kwa Dola za Marekani 122 milioni (Sh200 bilioni) akidai ni ufisadi uliofanywa na vigogo sita wa Serikali.

Aliwataja kwa majina vigogo hao na kusisitiza kuwa wamehusika na ufisadi wa fedha hizo zilizokuwa zimewekwa katika akaunti ya Baraza la Usuluhishi la Migogoro ya Kibiashara (Escrow), katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Akaunti hiyo ilifunguliwa kutokana na mgogoro wa kibiashara kati ya IPTL na Tanesco na Tanesco ilipeleka shauri hilo mahakamani kulalamikia gharama kubwa za uwekezaji wanazotozwa na IPTL, hivyo kuamuliwa fedha hizo ziwekwe humo hadi shauri litakapoamuliwa, lakini baadaye zilichotwa katika mazingira ya kutatanisha.

Lugola
Lugola aliibuka Mei 10, mwaka huu katika mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika na kusema kuwa Serikali ya CCM ambayo yeye ni mbunge wake, inaendeshwa kisanii huku akishangaa waziri mwenye dhamana ya kilimo, Christopher Chizza kuendelea kuwa waziri wakati hotuba yake imejaa blaablaa.

Pia alimgeukia Naibu Waziri, Godfrey Zambi na kumwambia amejisahau kwamba naye alikuwa akikaa kiti cha nyuma bungeni akipaza sauti, baada ya kupata madaraka amewageuka wenzake na kushirikiana na waziri.

Akizungumza kwa sauti ya ukali ambayo mara nyingi haitarajiwi kwa wabunge wa CCM, Lugola alihoji inakuwaje wakulima wanapelekewa pembejeo feki, dawa feki na skimu za umwagiliaji zinachakachuliwa na bado Chizza anaendelea kubaki kama waziri?
 
Keissy
Mei 27, mwaka huu ilikuwa zamu ya Keissy, mbunge machachari wa Nkasi Kaskazini pale alipozua sokomoko wakati akichangia hotuba ya Wizara ya Mambo ya Nje. Kauli yake kuwa Zanzibar haichangii katika Muungano hivyo haina haki ya kuhoji mambo ya upande wa pili wa Muungano na kwamba hata umeme hailipi nusura imponze.

Alisema Zanzibar ina asilimia 2.8 ya watu wote wa Tanzania na kwamba kwa idadi hiyo, wananchi wa jimbo moja wanaweza kukusanyika eneo moja kwa kuitwa na mlio wa filimbi tu, kauli iliyosababisha wabunge kutoka Zanzibar kutaka kumpiga ‘kavukavu’.

Abass Mtemvu
Juni 5, Mtemvu naye aliibua mpya baada ya kumlipua Mbunge wa Urambo Magharibi (CCM), Profesa Juma Kapuya kuwa anafahamu uuzaji wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (Uda) ambalo alidai limeuzwa kwa Sh280 milioni.

Mtemvu alisema kulifanyika ujanjaujanja kati ya Kampuni ya Simon Group na Meya wa Jiji Dar es Salaam, Didas Masaburi kukopa benki na taasisi nyingine kwa ajili ya kununua shirika hilo, kauli ambayo ilipingwa na Kapuya huku suala la Uda likiendelea kukamata mjadala hadi Mwendeshaji wa Uda kuitwa bungeni.

Faustin Ndungulile
Mei 29 mwaka huu, Dk Ndugulile alimweka katika wakati mgumu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka wakati wa mjadala wa bajeti ya wizara hiyo na kuwa Serikali haijashirikisha wadau katika mradi wa Kigamboni utakaogharimu Sh11.7 trilioni.

Sakata hilo liliingiliwa na Waziri Mkuu ambaye alisema kuwa tatizo la mradi huo ni elimu kutotolewa kwa umma na kuomba wabunge waiachie Serikali suala hilo.

Tundu Lissu
Juni 2, Lissu aliwalipua Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk Binilith Mahenge kwamba wanatumia vibaya nafasi zao kwa kuweka fedha nyingi za miradi ya maji katika maeneo wanakotoka, huku sehemu zenye matatizo ya huduma hiyo zikitengewa fedha kiduchu.

Lissu alisema Profesa Maghembe ambaye ni Mbunge wa Mwanga, Kilimanjaro, wizara yake imetenga Sh1.4 bilioni kwa ajili ya miradi ya maji, ambazo ni zaidi ya mara saba ya Sh190 milioni zilizotengwa kwa ajili hiyo katika Wilaya ya Ikungi, Singida.

Mawaziri hao waliokolewa na Profesa Mwandosya akisema kuwa miradi hiyo katika wilaya za Same, Mwanga na Korogwe ilianza wakati yeye akiwa Waziri wa Maji, hivyo hawakujipendelea.

Cecilia Paresso
Mbunge huyu aliichachafya Serikali na kuungwa mkono na wabunge 13 wanawake wakati akichangia Bajeti ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii wakitaka iongezewe fedha ili kukabiliana na vifo vya kinamama na watoto.

Paresso alisema wizara hiyo imetengewa Sh622 bilioni, ikiwa ni pungufu ya Sh131 bilioni ya bajeti ya wizara hiyo mwaka 2013/14 ilipotengewa Sh753 bilioni.

Hoja hiyo iliwanyanyua Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, Waziri wa Afya, Dk Seif Rashid na Naibu Mawaziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba na Adam Malima kutoa ufafanuzi. Wote hao walishindwa kumshawishi Paresso na wenzake, hadi Serikali ilipoahidi kuongeza fedha za wizara hiyo, ikiwa ni pamoja na kutoa Sh87 bilioni kwa ajili ya kulipa deni la Bohari Kuu ya Dawa (MSD).

CHANZO: MWANANCHI

Wednesday, 14 May 2014

Milioni 500/- zatengwa kukabili dengue

Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Kebwe Stephen Kebwe
Serikali  imetenga Sh. milioni 500 kwa ajili ya kunyunyiza dawa za kuua mazalia ya mbu kwenye maeneo chepechepe jijini Dar es Salaam, katika jitihada za kukabiliana na ugonjwa wa dengue.

Vile vile, imewaagiza watendaji wa vitongoji kusimamia usafi kwenye maeneo yao.

Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Kebwe Stephen Kebwe, aliyasema hayo wakati alitoa kauli ya serikali bungeni jana kuhusu ugonjwa wa homa ya dengue, baada ya Mbunge wa Kigamboni ( CCM), Dk. Ndugulile Faustine, kutaka taarifa ya serikali kuhusu hatua ilizochukua kudhibiti ugonjwa huo.

Dk. Kebwe alisema Wizara imeandaa mpango wa namna ya kukabiliana na ugonjwa huo na kwamba umeshirikisha sekta mbalimbali na kwamba hadi sasa zaidi ya Sh. milioni 132 zimetumika kwa ajili ya ugonjwa huo na kwamba fedha zaidi zitaendelea kutolewa.

“Wananchi wanashauriwa kutokuwa na hofu kuhusu ugonjwa huu kwani hauambukizwi kwa kumhudumia mgonjwa au kwa kugusa maji maji yanayotoka kwa mgonjwa...tunawashauri wananchi kwenda vituo vya afya haraka pindi waonapo dalili za ugonjwa huo,” alisema.

Alisema sehemu kubwa ya ugonjwa huo inachochewa na mazingira machafu na kwamba mvua kubwa zinazoendelea kunyesha zinachangia kuongezeka kwa mazalia ya mbu na kwamba utupaji, uzoaji na uhifadhi wa taka katika miji nchini hauridhishi hali inayotoa fursa kwa mazalia ya mbu kuongezeka.

Dk. Kebwe alisema hadi sasa hakuna chanjo wala dawa maalum kwa ajili ya kudhibiti au kutibu ugonjwa huo na kwamba njia kubwa ni kumzuia binadamu asiumwe na mbu.

USHAURI
Alisema mbinu shirikishi za kutokomeza mbu lazima zitiliwe mkazo na kwamba njia bora na rahisi ni kutokomeza mazalia yote ya mbu.

Pia, alisema watu wavae nguo zinazofunika mikono na miguu na kutumia dawa zinazofukuza mbu, watoto walale kwenye vyandarua vyenye viatilifu wakati wa mchana.

JINSI YA KUJIKINGA
Alisema njia ya kujikinga ni kufukia madibwi ya maji yaliyotuama au kunyunyuzia viuatilifu vya kuua viluwiluwi vya mbu kwenye madibwi, kuondoa vitu vinavyoweza kuweka mazalio ya mbu kama vifuu vya nazi, makopo, magurudumu ya magari na kufyeka vichaka karibu na makazi.

Nyingine ni kuhakikisha maua yanayopadwa kwenye makopo au ndoo hayaruhusu maji kutuama, kufunika mashimo ya majitaka kwa mfuniko imara na kusafisha grata za paa la nyumba ili kutoruhusu maji kutuama.

HATUA ZILIZOCHUKULIWA

Alisema timu ya taifa ya masafa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ikiwamo halmashauri za Jiji la Dar es Salaam na wadau wa maendeleo wanakutana kila mara baada ya wiki mbili kutathmini mikakati ya kamati ya dharura iliyowekwa.

Nyingine alisema serikali ilitoa tamko kuanzia Machi, mwaka huu, kuendelea kutoa taarifa ya taadhari ya ugonjwa huo kupitia kwa waganga wakuu wa mikoa na wilaya, ikiwa ni pamoja na namna mgonjwa anavyoweza kutambuliwa, mwongozo kwa watumsihi wa afya wa namna ya kuchukua sampuli, vipeperushi vinavyoelezea jinsi ya kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huo.

Pia, kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kupitia redio na runinga na kwamba wizara kwa kushirikiana na halmashauri za jiji wameendelea kutumia maafisa afya wakiwamo wa kata na uongozi wa mitaa kuwaelimisha wananchi namna ya kudhibiti ugonjwa kwa kutumia vipaza sauti.

Dk. Kebwe, alisema hatua nyingine ni kutoa elimu ya afya kwa watumishi wa afya pamoja na madaktari na mafundi sanifu wa maabara namna ya kutambua ugonjwa huo katika hospitali za Muhimbili, Amana, Mwananyamala na Temeke.

HALI ILIVYOKUWA JANA

Hospitali kadhaa jijini Dar es Salaam zimeendelea kupokea wagonjwa kwa mujibu wa taarifa za jana.

MWANANYAMALA
Juzi mgonjwa mmoja aligunduliwa na kutibiwa kisha kuruhusiwa na kufanya idadi ya wagonjwa waliothibitishwa kuugua ugonjwa huo katika hospitali hiyo kuwa 140.

Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Faustinias Ngonyani, alisema jana kuwa wagonjwa wote walitibiwa na kuruhusiwa.

Alisema ugonjwa huo ulipolipuka walipokea wagonjwa 139 na mmoja aliongezeka juzi na idadi ya wagonjwa 140 ambamo alisema kati yao wagonjwa sita ni watumishi wa hospitali hiyo, ambao hali zao zinaendelea vizuri.

AGA KHAN

Hospitali ya Aga Khan  imesema kwa wiki moja wamepokea wagonjwa 26, kati yao 17 walitibiwa na kuruhusiwa huku tisa wakiwa wamelazwa.

Muuguzi Mkuu wa hospitali hiyo, Loveluck Mwasha, alisema waliolazwa ni Wachina saba na Watanzania wawili na kuwa hali zao zikiendelea vizuri.

MUHIMBILI
Katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) jana alikuwapo mgonjwa mmoja.

Kwa mujibu wa Afisa Uhusiano Mwandamizi wa MNH, Aminieli Eligaesha, mgonjwa huyo alikuwa amelazwa kwenye kitengo cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi wa karibu (ICU) cha hospitali hiyo na alikuwa anafanyiwa vipimo ili kujua ugonjwa unaomsumbua ingawa dalili za awali zilionyesha kuwa anasumbuliwa na dengue.

TEMEKE
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Temeke, Dk. Amani Malima, alisema idadi ya wagonjwa katika hospitali yake imeongezeka na kufikia 20 na kuwa kati yao wapo watumishi 10 wa wilaya hiyo.

DK. BUBERWA AAGWA KWA MAJONZI

Vilio na simanzi vilitawala jana wakati wakuagwa kwa mwili wa Dk. Gilbert Buberwa (36) katika Hospitali ya Temeke jijini Dar es Salaam ambaye alifariki Jumapili iliyopita kwa ugonjwa wa dengue.

Dk. Buberwa ambaye alikuwa daktari bingwa wa magonjwa ya akili, alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Wafanyakazi wa Hospitali ya Temeke pamoja na madaktari wengine  walijikuta wakitokwa na machozi wakati wakiuaga mwili huo, huku wengine wakionekana kuwa na majonzi.

Mwakilishi wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, ambaye ni mtaalamu wa magojwa ya akili, Dk. Ayubu Magimba, alisema serikali imepata pigo kubwa kwa kifo cha  Dk. Buberwa kwa kuwa alikuwa akitegemewa kwa kiasi kikubwa.

Alisema wanasikitika kumpoteza mtu ambaye alikuwa ni makini na kwa mkoa wa Dar es Salaam alikuwa akitegemewa sana.

Hata hivyo, Dk. Magimba, alishindwa kuendelea kuzungumza kutokana na kutokwa na machozi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana baada ya kuagwa kwa mwili huo, Mganga Mkuu wa Hospitali ya Temeke, Dk. Amani Malima, alisema hospitali yake imepata pigo kubwa kwani walikuwa wakimtegemea kila idara.

“Dk. Buberwa alikuwa kichwa, pia alikuwa ni msaidizi wangu licha ya kwamba ni daktari bingwa wa masuala ya akili alikuwa na uwezo wa kuangalia idara zote na hata wodi za wanawake alikuwa akitibu hakuna kilichokuwa kinamshinda, hivyo hata nikiondoka ninakuwa sina wasiwasi kwa kuwa nimeacha jembe langu,” alisema Dk. Malima.

Dk. Malima alisema mwili wa marehemu umepelekwa nyumbani kwake Kinyerezi, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika leo.

 
CHANZO: NIPASHE

CCM lawamani mchakato Katiba mpya

Imeelezwa kuwa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), haina nia yoyote njema ya kusimamia mchakato na kuhakikisha Watanzania wanapata  Katiba mpya itakayotokana na mawazo yao kwa kuwa inaogopa lawama za kuvunja Muungano.

Kadhalika, imeelezwa kwamba mtu pekee ambaye ataweza kunusuru mchakato wa kupata Katiba mpya ni Rais Jakaya Kikwete.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), James Jesse, aliyasema hayo jijini Dar es Salaam alipozungumza na waandishi wa habari katika ofisi za Kituo Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).

"Ninaamini Rais Kikwete alikuwa na nia njema ya kuacha historia ya kuandika  Katiba mpya, lakini kwa bahati mbaya amezidiwa nguvu kutoka ndani ya chama chake CCM," alisema Jesse.

Alisema kama mchakato wa kujadili rasimu iliyotolewa na Jaji mstaafu, Joseph Warioba, ungeachwa ukaenda kama ulivyokuwa umepangwa bila kuingiliwa, kusingekuwa na migogoro ndani ya Bunge la Katiba.

Alifafanua kuwa endapo Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), wataendelea kukaidi kuingia katika Bunge la Katiba, hakuna kitu chochote kitakachoamuliwa kwa kuwa upande wa Zanzibar kura zikipigwa hawatafikia theluthi mbili ya kura zote.

"Hata ingekuwaje, Bunge la Katiba haliwezi kupitisha maamuzi yoyote ya sura za rasimu ikiwa Ukawa watakuwa nje hususani wajumbe wa kule Zanzibar," alisisitiza.

Jesse alisema ili wajumbe wa CCM wapitishe maamuzi, wanatakiwa kushinikiza sheria ibadilishwe ili watumie mfumo wa nusu ya kura zitakazopigwa badala ya theluthi mbili, jambo ambalo alisema litazua maswali mengi.

Aliongeza kuwa Watanzania wasilaumu Ukawa kukaidi kuendelea na mjadala wa Bunge la Katiba, badala yake wajiulize sababu za msingi zilizowafanya watoke nje.

"Profesa Lipumba ni msomi na mtu mwenye akili timamu, asingeweza kutoka nje bila sababu za msingi, kuna mambo ya misngi wanayotaka yatekelezwe lakini wanashindwa kutokana na uchache wao,'' alisema.

Aliongeza: "CCM hawashindi kutokana na hoja zao kuwa na maana ama nzuri bali wanatumia nguvu ya hoja kutokana na wingi wao na hawa Ukawa wanashindwa hata kama wana hoja nzuri kiasi gani kutokana na uchache wao," alifafanua.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati Maalum ya Katiba ambayo ipo chini ya LHRC, Dk. Koti Kamanga, alisema Bunge la Katiba limevurugwa na wanasiasa ambao wanaendekeza itikadi za vyama vyao.

Alisema serikali haina nia njema ya kupatikana Katiba mpya kwa kuwa imevunja Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kwamba hatua hiyo inadhoofisha mchakato mzima kwa kuwa kukitokea mkanganyiko wa hoja znazojadiliwa hakuna mtu atakayezijibu.

CHANZO: NIPASHE

Zaidi ya wachimba migodi 200 wafa Uturuki

Wachimba migodi wakisaidia kwenye juhudi za uokozi wa wenzao waliokwama kwenye mgodi wa makaa ya mawe wa Soma, kusini mwa Instanbul.
Uturuki imetangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa huku idadi ya waliokufa kwenye mripuko uliotokea katika moja ya ajali mbaya kabisa kuwahi kutokea kwenye sekta ya madini nchini humo ikipindukia watu 200.

Bendera ya Uturuki ndani na nje ya nchi hiyo inapepea nusu mlingoti kuomboleza msiba huo mkubwa, huku zaidi ya watu 300 wakiendelea kukwama chini ya ardhi katika mji wa Sama ulio kwenye jimbo la Manisa.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Ujerumani, dpa, wakati moto uliporipuka usiku wa kuamkia leo, kwenye mgodi huo kulikuwa na watu 787.

Vikosi kadhaa vya uokoaji vinashiriki kwenye uokozi na Waziri wa Nishati wa Uturuki, Taner Yiildiz, amesema hadi sasa watu waliokolewa ni 365:


"Operesheni za uokoaji zinaendelea. Hadi sasa tumeshapoteza wachimba madini wetu 201. Tunahofia kwamba idadi inaweza kuongezeka. Nilisema pia kwamba kuna kiasi cha watu 80 waliojeruhiwa, 60 kati yao wakiwa ni wachimba madini." Alisema Waziri Yiildiz akiwa nje ya mgodi huo.


Vifo hivyo vimesababishwa na hewa ya sumu inayotokana na moto. Hadi asubuhi ya leo, bado moto huo unaosemekana kusababishwa na hitilafu za umeme, ulikuwa ukiendelea kuwaka, masaa 18 baada ya mripuko kutokea.

Waziri Yiildiz pia amesema kuwa baadhi ya wafanyakazi wako umbali wa kilomita mbili chini ya ardhi na usawa wa kilomita nne kutoka lango kuu la kutokea, jambo linalokwamisha jitihada za uokozi. Waandishi wa habari wanasema wachimba madini hao hawakuweza kutumia lifti kujiokoa kwani mripuko huo ulikuwa umekata kabisa umeme mgodini humo.

Waziri Yiildiz pia amesema kuwa baadhi ya wafanyakazi wako umbali wa kilomita mbili chini ya ardhi na usawa wa kilomita nne kutoka lango kuu la kutokea, jambo linalokwamisha jitihada za uokozi. Waandishi wa habari wanasema wachimba madini hao hawakuweza kutumia lifti kujiokoa kwani mripuko huo ulikuwa umekata kabisa umeme mgodini humo.

Waziri Mkuu Tayyip Erdogan ameahirisha ziara yake ya kikazi nje ya nchi na anatazamiwa kulitembelea eneo hilo la ajali, lililo umbali wa kilomita 250 kusini mwa mji mkuu Istanbul.

Kampuni ya Soma Holding inayomiliki mgodi huo imesema mgodi wao ulifanyiwa majaribio ya usalama miezi miwili iliyopita, lakini vyombo vya habari nchini Uturuki vimeripoti kwamba chama tawala cha AKP kilikataa wito wa upinzani bungeni, kutaka mgodi wa Soma kuhakikiwa mwezi uliopita.

Uturuki ina historia ya ajali mbaya za migodini, inayochangiwa na kanuni mbaya za usalama. Mwaka 1992, ajali kama hiyo iliua zaidi ya watu 260 katika mgodi ulio karibu na Bahari Nyeusi

CHANZO: DW.

Dk Shein akataa kuongeza posho BLW

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt, Ali Mohammed Shein.
Zanzibar. Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amekataa maombi ya kuwaongezea posho wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW) kutoka Sh150,000 hadi Sh200,000.

Uamuzi huo wa Dk Shein umetokana na hali ya uchumi Zanzibar kutoruhusu nyongeza hiyo kwa sasa.

Katibu wa BLW, Yahya Khamisi Hamad alithibitisha jana kuwa baraza hilo lilipeleka kwa Rais Shein maombi la kutaka posho ya vikao hivyo iangaliwe upya kutokana na sababu mbalimbali, lakini kulingana na mazingira ya hali ya uchumi ilivyo kwa wakati huu imeshindikana kufanya hivyo.

Hamad alisema Dk Shein amewataka wajumbe kuwa na subira kwa kipindi hiki hadi hali itakaporuhusu kiuchumi na suala hilo linaweza kufikiriwa.

Alisema Dk Shein alitoa msimamo huo alipokutana na Spika wa baraza hilo, Pandu Ameir Kificho kwa nia ya kumweleza uamuzi kuhusu suala hilo. “Rais amekataa maombi ya nyongeza ya posho za vikao vya wajumbe wa BLW kutokana na hali ya mazingira ya kiuchumi kutokuwa mazuri kwa wakati huu, amewataka wawe na subira hadi hali ya mambo itakapotengamaa,” alisema Hamad.

Alisema kamati ya uongozi ya baraza hilo tayari imekwishataarifiwa kuhusu maombi ya posho kukataliwa na wajumbe wote kutoka CCM na CUF walitarajiwa kutaarifiwa jana kuhusu uamuzi huo.

Wajumbe hao wamekuwa wakilipwa posho ya Sh 150,000 kwa siku mbali na mshahara na posho nyingine zinazokaribia Sh4,500,000 kwa mwezi.

Akizungumzia kikao cha bajeti kinachoanza leo mjini Zanzibar, Hamad alisema kikao hicho kitalazimika kupunguzwa kwa siku ili kuwahi Bunge Maalumu la Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linalofanyika Dodoma ambalo lipo likizo na linatarajiwa kukutana Agosti 5.

Alisema kwa mujibu wa ratiba, kikao cha bajeti kinatarajia kutumia siku 56, tofauti na miaka mingine ili kukimbizana na muda na kuwataka wajumbe kujadili bajeti ili kuokoa muda na kuwahi Bunge la Katiba.

Aidha, katibu huyo wa BLW alisema kikao hicho kitakuwa na maswali 90, miswada miwili ya sheria ukiwamo wa Sheria ya Fedha na ule wa Sheria ya Kuidhinisha Matumizi ya Serikali mwaka 2014/2015.

Tayari, Waziri wa Fedha, Omar Yussuf Mzee amesema SMZ katika mwaka huu wa fedha inatarajia kutumia Sh 705.1 bilioni, kati ya hizo, makusanyo ya Serikali yatakuwa ni Sh 399 bilioni na kiasi kingine cha Sh 305.3 bilioni ni misaada ya wahisani na mikopo mbalimbali.

CHANZO: MWANANCHI.

Waziri akwepa hoja, amshambulia Lissu

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Hassan Suluhu akiwasilisha bunge makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira kwa mwaka fedha 2014/15, mjini Dodoma jana.
Dodoma. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), Samia Suluhu Hassan alikataa kueleza walipo waasisi sita wa Muungano ambao kambi ya upinzani ilidai kuwa waliuawa na kuzikwa handaki moja, badala yake akatumia nafasi hiyo kumshambulia mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu akidai hizo ni propaganda na upotoshaji.

Juzi wakati akiwasilisha hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani, Lissu aliitaka Serikali kutoa maelezo bungeni kuhusu sababu za kuuawa kwa waasisi sita wa Muungano wa Tangayika na Zanzibar na kuzikwa katika handaki moja visiwani Zanzibar.

Lissu aliwataja waasisi hao kuwa ni Abdalah Kassim Hanga, aliyekuwa waziri mkuu, Abdul Aziz Twalam aliyekuwa Waziri wa Fedha na Abdulaziz na Saleh Akida aliyekuwa mjumbe wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar.

Pia aliwataja Othman Shariff, Mdungi Ussi na Jaha Ubwa ambao alisema nao waliuawa na kuzikwa katika handaki moja eneo la Kama nje kidogo ya Zanzibar.

“Tunataka kujua ukweli kama walifanya makosa, walishtakiwa katika mahakama gani iliyowahukumu adhabu ya kifo... tunataka kuambiwa ukweli kwanini mchango wao kuhusu Muungano umefichwa,” alisema Lissu juzi.

Lakini alipoulizwa kuhusu madai hayo, Waziri Hassan alionekana kuzigeuza hoja hizo kuwa ni za Lissu pekee badala ya kambi ya upinzani na kumshambulia mbunge huyo akidai kuwa ni mpotoshaji, anayepiga propaganda na mchochezi.

Waziri huyo, ambaye ni Mzanzibari, alisema alipuuza maswali yote kuhusu waasisi hao akisema mbunge huyo wa Chadema alipotoka katika hotuba yake na ndio maana hakutaka kuzungumzia katika majumuisho ya bajeti ya ofisi yake bungeni.

“Yule Lissu sio mkweli na ndio maana sisi tulimpuuza,” alisema waziri huyo.

“Hakuna kitu kama hicho na endapo kingekuwepo sisi Serikali tungeshatoa ufafanuzi ili watu wapate kujua ukweli wake,” aliongeza Waziri Samia bila kutoa ufafanuzi wa nini kiliwatokea watu hao walioshika nafasi za juu serikalini mara baada ya Mapinduzi na Muungano wa Zanzibar na Tanganyika.

Pamoja na kudai kuwa aliona hoja hizo ni upotoshaji, Waziri huyo, ambaye pia ni makamu mwenyekiti wa Bunge la Katiba, aliwasihi wabunge wa upinzani kupeleka hoja zao katika Bunge Maalumu la Katiba linalojadili uundwaji wa Katiba Mpya, ambalo pia limetawaliwa na suala la muundo wa Muungano na kero zake.

Waziri Samia alisema hoja hizo zinalenga kuwaaminisha Watanzania mambo ambayo hayapo ili kuwajaza chuki dhidi ya Serikali yao na pia alidai zina uchochezi ndani yake.

Waziri Samia aliwashauri wabunge pamoja na Watanzania kupuuza kauli hizo akidai mbunge huyo hautakii mema Muungano na ndio maana anaibua mambo aliyodai kuwa ni ya uongo na ya uchochezi.

Madai ya Lissu

Lissu alitoa madai hayo akinukuu kitabu cha Kwaheri Ukoloni, Kwaheri Uhuru kilichoandikwa na Harith Ghassany ambacho kinaonyesha jinsi ambavyo viongozi hao wa SMZ waliuawa na kuzikwa katika kaburi moja.

“Sisi wa kizazi cha Muungano tunataka kujua ukweli juu ya makosa waliyoyafanya hawa waasisi wa Muungano hadi wakauawa na kuzikwa katika kaburi au handaki moja,” alisema Lissu.

Jitihada za kumpata Makamu wa Pili wa Rais wa SMZ, Balozi Seif Ali Idd na Waziri wa Nchi katika ofisi yake, Mohamed Abood kuzungumzia msimamo wa SMZ kuhusu kauli hiyo hazikuzaa matunda kwa kuwa simu zao ziliita bila majibu.

Akizungumzia suala hilo, mbunge wa viti maalumu, Anna Abdallah alisema naye alidai hoja hizo za Lissu ni za uchochezi ambao usipopuuzwa, unaweza kusababisha chuki kwa jamii.

“Ule ulikuwa ni uchochezi, na upinzani wa aina hiyo ni wa ajabu sana… kwa mtazamo wake yeye anafikiri anawafurahisha Wazanzibari, lakini wamemuona ni mtu wa ajabu,” alisema mwanasiasa huyo mkongwe.

Pamoja na uzito wa tuhuma hizo, baadhi ya wabunge waliohojiwa na gazeti hili jana walionekana kuzungumza kimkakati kwamba hawakusikiliza hotuba hiyo.

Utata mkubwa bado umezunguka kutoweka kwa Hanga na wenzake machapisho mbalimbali yanawatambua kama watu waliokuwa mstari wa mbele katika Mapinduzi ya Zanzibar na ambao waliunga mkono Muungano mara baada ya mapinduzi hayo.

CHANZO: MWANANCHI

Tuesday, 13 May 2014

Pacha wazaliwa wakishikana mikono Marekani

Mama wa mapcha hawa amesema mapacha wake ni zawadi kubwa kwake
Mama mmoja nchini Marekani, amejifungua watoto pacha wakiwa wameshikana mikono.
Watoto hao pia walikuwa wanapumua bila usaidizi wowote walipotolewa kutoka katika mashine yenye hewa ya Oxygen.

"Tayari wanaonekana kuwa marafiki ,’’ alisema mama yao Sarah Thistlethwaite.Mama wa watoto hao, alisema kuwa watoto hao waliopewa majina ya Jillian na Jenna Thistlewaite walikuwa wameshikana katika kitovu na kutumia Kondo moja la nyuma , hali ambayo madaktari walisema ni nadra.
Walizaliwa Ijumaa katika jimbo la Ohio, wakiwa wameshikana mikono.
Inaarifiwa ni mama mmoja tu kati ya akina mama elfu kumi mwenye uwezo wa kujifungua watoto pacha wa aina hiyo.
Bi Thistlewaite, mwenye umri wa miaka 32,alilazimika kupumzika kwa wiki kadhaa kabla ya kujifungua kwani pacha wanaozaliwa wakiwa wameshikana mikoni ni hali nadra ambayo inaweza kuhatarisha maisha ya watoto na mama kabla ya kuzaliwa.
Mama huyo alisema kupokea watoto wake ilikuwa zawadi tosha kwake wakati huu wa kusherehekea siku ya akina mama duniani.